Header Ads

ad

Breaking News

Yanga mwendo mdundo, yaipiga Polisi Moro 3-0



Yanga hao


Na Mwandishi Wetu

YANGA wameendeleza wimbi la ushindi katika mechi zao za hivi karibuni za Ligi Kuu Tanzania Bara, baada ya kuichapa Polisi Morogoro mabao 3-0, katika mchezo uliopigwa jana kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, leo.

Pamoja na ushindi huo, Yanga imeendelea kushika nafasi ya tatu katika ligi hiyo kwa kufikisha pointi 17, ikiwa nyuma ya vinara Simba wenye pointi 19 sawa na Azam wanaoshika nafasi ya pili kutokana na kuzidiwa idadi ya mabao na Wekundu wa Msimbazi hao.

Yanga walioanza vibaya ligi hiyo kwa kutoka suluhu na Prisons ya Mbeya ugenini kabla ya kupokea kipigo cha mabao 3-0 ugenini kwa Mtibwa Sugar ya Morogoro, jana walipata bao la kwanza katika dakika ya tano kupitia kwa Simon Msuva aliyetumia vyema pasi maridadi ya Jerryson Tegete.

Dakika moja baadaye, mshambuliaji wa Yanga kutoka Burundi, Didier Kavumbagu, aliipatia Yanga bao la pili baada ya kuwatoka mabeki wa Polisi Morogoro na kipa wao, Manji Kulwa na kuukwamisha mpira nyavuni.

Mganda Hamis Kiiza aliyetokea benchi kuchukua nafasi ya Tegete, aliifungia Yanga bao la tatu dakika ya 56, baada ya kuunganisha krosi iliyochongwa na David Luhende kutoka wingi ya kushoto.

Msuva nusura aipatie Yanga bao la nne dakika ya 68, pale alipopata mpira akiwa ndani ya eneo la hatari na kupiga shuti lililombabatiza kipa wa Polisi Morogoro aliyechukua nafasi ya Kulwa, Kondo Salum, na kumrudia na kupiga tena fyongo iliyookolewa na kipa huyo kwa mara nyingine na kuwa kona butu.

Polisi Morogoro walipata nafasi za kufunga katika dakika za 30, 54, 74 na 87 kupitia kwa washambuliaji wao, Malimi Busungu, Mokili Rambo na Nicholas Kabipe, lakini walishindwa kuzitumia kupata mabao kutokana aidha na umakini wa kipa wa Yanga, Ally Mustapha ‘Barthez’ au kujichanganya kwao.

Kwa ujumla, Yanga waliwazidi Polisi Morogoro kila idara katika mchezo huo ulioonekana kuwa wa upande mmoja, hasa katika kipindi cha pili.

Kwa upande wao, Polisi Morogoro walijitahidi kufurukuta kipindi cha kwanza, lakini katika kipindi cha pili, timu hiyo ilionekana kusambaratika na kupoteana hivyo kuwapa nafasi Yanga kujinafasi kadri walivyotaka.

Iwapo washambuliaji wa Yanga wangekuwa makini zaidi, wangepata mabao mengi zaidi katika mchezo huo, kwani walikuwa wakipata nafasi lukuki ambazo hata hivyo walishindwa kuzitumia ipasavyo, ama kutokana na papara au uchoyo wa kupeana pasi wao kwa wao kuelekea lango la Polisi Morogoro.

Yanga:  Ally Mustapher ‘Barthez’, Shadrack Nsajigwa, Oscar Joshua, Mbuyu Twite, Nadir Haroub ‘Cannavaro, Athuman Idd ‘Chuji’, Simon Msuva, Haruna Niyonzima/Nurdin Bakari, Jerry Tegete/Hamis Kiiza, Didier Kavumbagu na David Luhende/Nizar Khalfan.
Polisi Moro: Manji Kulwa/Kondo Salum, Nahodha Bakari, John Bosco, Noel Msakwa, Salmin Kisi, Hamisi Mamiwa, Bantu Admin, Paschal Maige, Mokili Rambo, Malimi Busungu na Nicholas Kabipe/ Keneth Masumbuko. 
Kutoka Uwanja wa Azam Complex Chamazi, Mwandishi Wetu anaripoti kuwa, mechi ya Ligi Kuu Tanzania Bara kati ya Azam FC dhidi ya Ruvu Shooting ilimalizika kwa sare ya bao 1-1.
Ruvu Shooting walikuwa wa kwanza kupata bao lililofungwa na Seif Abdallah, lakini Azam FC walisawazisha kupitia kwa mshambuliaji wao wa kimataifa, Kipre Tchetche, bao lililozifanya timu hizo kugawana pointi.
Kwa upande wa Ligi Daraja la Kwanza, Mbeya City imeichapa Burkina Faso bao 1-0, katika mechi iliyochezwa kwenye Uwanja wa Jamhuri, mjini Morogoro, jana.

ciao

No comments