Header Ads

ad

Breaking News

Yanga balaa, yaikamata Simba



Didier Kavumbagu (kushoto) na Ramadhan Malima wa Mgambo, wakiwania mpira, jana.

  Na Mwandishi Wetu

MABINGWA wa soka wa Afrika Mashariki na Kati (Kombe la Kagame), Yanga, jana imefanikiwa kukifikia kileleni mwa Ligi Kuu Tanzania Bara na Simba, baada ya kuicpiga Mgambo JKT mabao 3-0, mechi iliyopigwa Uwanja wa Taifa, Dar e Salaam, hivvo kufikisha pointi 23.

Pointi hizo zinaifanya timu hiyo kulingana na Simba waliotoka sare ya bao 1-1 na Polisi Morogoro kwenye Uwanja wa Jamhuri, mjini Morogoro jana.

Yanga imefanikiwa kulingana pointi na Simba, ikiwa ni baada ya mabingwa hao wa Afrika Mashariki na Kati, kuanza vbaya ligi hiyo kwa kutoka suluhu na Prisons mjini Mbeya, kabla ya kupokea kipigo cha mabao 3-0 kutoka kwa Mtibwa Sugar kwenye Uwanja wa Jamhuri, Morogoro.

Mwenendo huo wa kusuasua katika ligi hiyo, ulionekana kuwakera wapenzi wa timu hiyo na kuanza kukata tama ya timu yao kufanya vema kwenye ligi hiyo, huku watani wao wa jadi, Simba, wakiwakejeli kadri walivyotaka.

Lakini hatimaye wapenzi wa timu hiyo kwa sasa hawana shaka tena na maswali yao juu ya mwenendo wa timu yao, huenda yamepata majibu, kwamba uwezekano wa kutwaa ubingwa wa ligi hiyo ni mkubwa mno kutokana na kasi ya ‘chama’ lao hilo, wakiwa wameshinda mechi tano mfululizo.

Katika mchezo huo, Yanga walianza kuandika bao lao la kwanza katika dakika ya nne kupitia kwa beki wao, Nadir Haroub ‘Cannavo’, aliyeunganisha krosi ya beki mwenzake, Mbuyu Twite.

Bao hilo lilionekana kuwaamsha usingini Mgambo JKT ambao walijipanga na kupeleka mashambulizi kadhaa katika lango la Yanga, lakini safu ya ulinzi ya timu hiyo, ilikuwa imara kuondosha hatari hizo.

Wakicheza kwa usongo wa kufunga mabao zaidi, Yanag walipata bao la pili lililofungwa na mshambuliaji wao raia wa Burundi, Didier Kavumbagu katika dakika ya 41, akiunganisha vema krosi maridadi ya Mganda Hamis Kiiza ambaye naye alipokea pasi ya beki wa kushoto, Oscar Joshua.

Akiingia kutokea benchi katika dakika ya 68, Jerry Tegete, kwa mara nyingine alithibitisha umahiri wake wa kucheka na nyavu anapokuwa mbele ya lango, baada ya kuifungia Yanga bao la tatu dakika ya 80.

Baada ya bao hilo, Yanga walihaha kuongeza bao la nne ambalo lingewawezesha kushika usukani wa ligi hiyo kwa kuwa na idadi kubwa ya mabao ya kufunga, huku wastani wa mabao ya kufunga na kufungwa wakilingana na Simba, yaani mabao 12.

Pamoja na kufungwa, Mgambo JKT, walionesha kandanda ya hali ya juu, wakimiliki mpira na kuonana vilivyo, lakini walishindwa kufurukuta kwa kuzidiwa uzoefu na wakali hao wa Jangwani.

No comments