Header Ads

ad

Breaking News

Waziri Mwakyembe atengua uteuzi wa mwenyekiti BMT



                           
                                      Mwandishi Wetu

WAZIRI wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Harrison Mwakyembe ametengua uteuzi wa mwenyekiti na wajumbe wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT), baada ya kushindwa kupata ufumbuzi wa migogoro katika michezo nchini.


Maamuzi hayo yametolewa baada ya Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, hivi karibuni kumwagiza Waziri wa Michezo  kulipitia baraza hilo na iwapo hataridhika na utendaji wake, alivunje.

Leo, Waziri Mwakyembe amesema sekta ya michezo imekuwa na migogoro mingi inayochangia kushusha maendeleo ya michezo nchini. Mwenyekiti wa BMT alikuwa Dioniz Malinzi.

Amesema agizo hilo la Waziri Mkuu limekuja wakati sahihi, kwani alifanya kikao na BMT kulielimisha kuhusu wajibu wake kisheria, changamoto zinazolikabili baraza hilo na hali ya uhuru uliopitiliza katika uongozi wa uendeshaji wa michezo nchini.

Amesema pamoja na BMT kulalamikia ukosefu wa fedha kama kikwazo kikubwa kinachokwamisha utendaji kazi wake, wizara imeona zaidi hitaji la utashi, dhamira na kujituma kuliko fedha katika kutatua sehemu kubwa ya udhaifu unaotawala tasnia ya michezo.

Waziri Mwakyembe amezungumzia kasoro ya viongozi wa michezo kushika zaidi ya nafasi moja ya uongozi, vitu vinavyochangia kushusha kiwango cha michezo nchini, hata ushiriki wa michezo wa Tanzania nje ya nchi bila kulishikirisha baraza hilo.

Pia, amezungumzia mapromota wa mchezo wa ngumi kuendesha shughuli zao bila kusajiliwa, chaguzi za vyama vya michezo kugubikwa na ubabe na rushwa, katiba na kanuni za vyama kutohakikiwa kubaini upungufu kuhusu masuala ya fedha, tuhuma za rushwa, ubadhirifu, upendeleo na maamuzi ya kibabe.

Mambo hayo yamemfanya Waziri Mwakyembe kusema kuwa, baraza litafanya kazi kwa kushirikiana na wizara wakati taratibu za kumpata mwenyekiti na wajumbe wapya zikiendelea kufanyika kwa mujibu wa sheria.

No comments