Header Ads

ad

Breaking News

Azam safi, Mtibwa sare



AZAM FC, baada ya kuikosa Ngao ya Hisani kwa kufungwa na Simba mabao 3-2, Jumanne iliyopita, jana ilisawazisha mabao yake na kufanikiwa kuichapa Kagera Sugar bao 1-0.

Katika mechi hiyo ya ligi kuu Bara inayodhaminiwa na Kampuni ya Simu ya Vodacom, Azam walikuwa ugenini kwenye Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba, ambapo walifanikiwa kuwanyamazisha mashabiki wa timu hiyo waliokuwa wakiishangilia.

Bao pekee la Azam lilifungwa na Abdulhalim Humoud, na kuzima kabisa kelele za mashabiki wa Kagera Sugar waliokuwa wamejaa uwanjani.

Katika mchezo huo, Humoud alionesha kiwango kizuri cha soka, ambapo mashabiki waliokuwepo uwanjani, walikuwa wakisema kuwa, ni mchezaji bora wa mechi hiyo.

Kutoka Morogoro, Mtibwa Sugar na Polisi Morogoro, jana zilianza ligi kuu Bara kwa kugawana pointi, baada ya kutoka suluhu, katika mechi iliyopigwa kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro.

Katika mchezo huo, washambuliaji wa Mtibwa Sugar, Jamal Mnyate na Hussein Javu, walishindwa kutumia vizuri nafasi walizopata na kuinyima timu yao ushindi.

Hivyo, kwa matokeo hayo, timu hizo zote kutoka mkoani Morogoro, zimeambulia pointi moja.
Kutoka Tanga kwenye Uwanja wa Mkwakwani, Coastal Union imedhihirisha ubabe wake kwa Mgambo JKT, baada ya kuilaza bao 1-0, mechi iliyochezwa kwenye Uwanja wa CCM Mkwakwani jijini Tanga.

Bao pekee la Coastal Union lilifungwa na Jerry Santo, dakika ya 46, baada ya kupokea pasi safi kutoka kwa Juma Jabu na kuukwamisha mpira wavuni.

Kutoka jijini Mwanza,  Toto Africa na Oljoro JKT, zimegawana pointi baada ya kutoka sare ya bao 1-1, katika mechi ya Ligi Kuu Bara iliyochezwa kwenye Uwanja wa CCM Kirumba jijini hapa.

Toto walitawala mchezo kipindi cha kwanza, lakini dakika ya nne walishindwa kufunga bao kwa mkwaju wa penalti, baada ya Emmanuel Swita kupiga mkwaju huo na kupanguliwa vizuri na kipa Shaibu Issa wa Oljoro JKT.
Baada ya kukosa penalti hiyo, Oljoro walizinduka na kulisakama lango la wapinzani wao, ambapo Omar Issa alipata nafasi nzuri ya kufunga bao, lakini shuti lake lilitoka nje ya lango.

Toto walipata pigo baada ya beki wake wa kati, Evarist Maganga kuumizwa mdomoni na kukimbizwa hospitali, nafasi yake ikachukuliwa na Hussein Shaha.

Oljoro wakijibu mashambulizi, walipata nafasi nzuri dakika ya 85, lakini shuti la Omar Issa, lilipanguliwa na kipa kipa wa Toto, Emmanuel Ngwengwe, kabla ya mabeki kuuondoshwa katika hatari.

Mashambulizi ya Oljoro yalizaa matunda dakika ya 87, baada ya Hamad Omar kuipatia, lakini Mohamed Neto aliisawazishia Toto bao hilo dakika ya 87.

Kutoka katika Uwanja wa Azam Chamazi jijini Dar es Salaam, timu ya soka ya Ruvu JKT, jana ilianza vizuri ligi kuu Bara, baada ya kuilaza Ruvu Shooting mabao 2-1.

Mechi hiyo ilizikutanisha timu zote zinazomilikiwa na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), ambapo kila timu ilionesha kiwango kizuri uwanjani.

No comments