Header Ads

ad

Breaking News

Familia ya Mafisango yatupiwa virago nje


Mdogo wake, Joel Mafisango akiangalia vyombo vyao.

Na Mwandishi Wetu

FAMILIA  ya aliyekuwa kiungo mshambuliaji wa timu ya Mabingwa wa soka Ligi Kuu Bara, Patrick Mutesa Mafisango, jana wamejikuta wakitupiwa vitu vya marehemu Mafisango nje ya nyumba hiyo kwa kudai kuwa mkataba wa kuishi hapo umekwisha.

Familia hiyo imejikuta ikiwa katika wakati mgumu baada ya mkataba wa kuishi katika nyumba ambayo marehemu Mafisango alikuwa anaishi kumalizika ambapo ilidaiwa kulipwa na uongozi wa Simba.

Akizungumza na SuperStar jana, ndugu wa marehemu Mafisango, Joel Mafisango, alisema kuwa, kitendo kinachofanywa na uongozi wa Simba, si kizuri cha kuzuia kuuza mali za marehemu wakiwa kama ndugu wa marehemu.

“Uongozi wa Simba kutuzuia ndugu wa marehemu kuuza vitu si vizuri, sisi ni watu ambao tulikuwa tunaishi na marehemu na ni ndugu, iweje watuzuie kufanya hivyo,” alisema.

Alisema kuwa, kama Simba hawapo tayari kuruhusu kuuza vitu hivyo, basi wavisafirishe mpaka nyumbani kwa marehemu ili na wao waweze kuondoka, kwani wanaishi kwa shida.

“Kama wanatuzuia kuviuza vitu, tunaomba wawe na jukumu la kuvisafirisha mpaka nyumbani kwao marehemu, tunakaa hapa sababu ya vitu vya marehemu, ingawa Simba hawatujali, wala kufikiria mali za marehemu, mchezaji wao.

“Tunadhalilika kwa sababu ya timu ya Simba, na kama hawatafanya hivi ambavyo ndugu tunahitaji, basi wajue lazima watakwenda kwenye kaburi la marehemu Mafisango kule DR Congo kuomba msamaha, juu ya kaburi, kwa kitendo ambacho wametufanyia, vingenevyo Simba haiwezi kufika kokote kimaendeleo,” alisema Joel ambaye alionekana kusononeshwa na kitendo hicho.

Naye mmiliki wa nyumba hiyo, Chingweni Mtoro, alisema kuwa, mkataba wa marehemu Mafisango ulikuwa umemalizika Julai 28, mwaka huu na kudai kuwa,  uongozi wa Simba uliomba kuongezewa muda wa siku saba, ili waweze kushughulikia suala hilo.

“Julai 28, mwaka huu ndio ilikuwa mwisho wa mkataba, lakini baadhi ya wahusika wa Simba SC, akiwemo Kesi aliyemtaja kwa jina moja, alimwomba waongeze muda wa siku saba ili waweze kulipa kodi ya mwezi mmoja mbele.”

“Mpaka kufikia sasa, kila nikijaribu kuongea na uongozi huo kwa njia ya simu, naambiwa subiri, na huu ni mwezi wa nane,  sioni mwelekeo wowote wa kupewa change, hivyo naona bora niwafukuze ndugu wa marehemu Mafisango,” alisema.

Alisema kuwa, kwa sasa amepata mtu mwingine anayetakiwa kuingia kwenye nyumba hiyo, na ndio maana ameona njia pekee ni kuwaondoa ndugu hao.

“Kama wapo tayari kuondoka, nipo tayari kuwasaidia usafiri wa kubebea mizigo yao na kuipeleka kule ambako watakwenda kuishi kwa hapa Dar es Salaam, na hilo deni langu la sh. 350,000, ambalo ni la mwezi mmoja, nitawasamehe,” alisema Mtoro.

Familia hiyo ilikuwa ikiishi na marehemu Mafisango ambaye alifariki April mwaka huu, alikuwa akiishi na ndugu zake wanne akiwemo Joel.

Katika kujua ukweli wa jambo hilo,  gazeti hili liliweza kuzungumza na uongozi wa Simba kupitia kwa Makamu  Mwenyekiti wao, Geofrey Nyange ‘Kaburu’, ambaye alikiri kwamba,  mkataba wa pango kwenye nyumba hiyo iliyopo maeneo ya Keko jijini Dar es Salaam, umekwisha na kuwataka ndugu hao kurejea kwao kama hawana kazi ya kuwawezesha kuishi.

“Tunaweza kuwasaidia, lakini si wajibu wetu, notisi ilitoka na kati ya hao mmoja ambaye ni ndugu wa Mafisango, alikwenda hadi Kinshasa kuzika, lakini wengine ni ndugu wa kuunga unga na wanatoka maeneo ya Goma.

“Jambo la msingi warudi  makwao kama hapa hawana kazi ya kuwawezesha kuishi mjini, huyo wa Kinshasa ambaye ni ndugu wa marehemu tutampa nauli kama akiwa tayari kwa muda wake. Tatizo hawataki kurudi kwao na wanataka Simba iwape nyumba na fedha ya chakula, je, yanawezekana hayo? Alihoji Kaburu.

No comments