Header Ads

ad

Breaking News

Simba wawawekea pingamizi Yondani, Twite TFF

Kelvin Yondani

KLABU ya Simba imeweka pingamizi Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), la wachezaji wa Yanga, Kelvin Yondani na Mbuyi Twite, ambao wamesajili kwa ajili ya msimu ujao wa Ligi Kuu Bara.

Awali, mabingwa hao wa soka nchini, Simba, walidai kuwa, Yondani bado ni mchezaji wao, kwani ana mkataba nao, huku wakidai Twite, ambaye amesajiliwa na Yanga akitokea APR ya Rwanda, ni mchezaji wao pia.  

Simba walimsajili Twite siku chache, baada ya kumalizika kwa michuano ya Kombe la Afrika Mashariki na Kati, ambapo kwa upande wa beki wake wa zamani Yondani, aliamua kutimkia Yanga, licha ya kuwa na mkataba na Simba wa mwaka mmoja.

Akithibitisha taarifa hizo, Ofisa wa Habari wa Simba, Ezekiel Kamwaga, alikiri kupeleka pingamizi hilo, baada ya pazia la usajili wa ligi kuu kwa wachezaji wa ndani kufungwa.
“Kweli tumepeleka pingamizi TFF kuwapinga wasichezee Yanga, kutokana Simba kuwa na mikataba nao,” alisema Kamwaga.

Kwa upande mwingine, Kamwaga alisema uongozi wa Simba umewasilisha pingamizi lingine la kutokuwa na imani na Kamati ya Katiba Sheria, Maadili na Hadhi za wachezaji.
Kamwaga alisema Simba imefikia hatua hiyo ya kuipinga kamati hiyo iliyo chini ya Alex Mgongolwa, kutosikiliza pingamizi hilo kutokana na wajumbe wake kuwa na mapenzi na Yanga.

Kiongozi huyo wa Simba alisema kabla ya kamati hiyo kusikiliza shauri hilo, Mgongolwa alisikika akusema kuwa, katika mkataba wa Simba na Yondani, una mapungufu.
Kamwaga alisema kauli ya mwenyekiti huyo imewapa hofu na hivyo kutokuwa na imani katika kusikiliza pingamizi hilo.

Wajumbe wengine waliowekewa pingamizi kutosikiliza shauri la Yondani na Twite ni Imani Madega, Lloyd Nchunga na Omary Gumbo.

Akitaja sababu za kuwawekea pingamizi ni kutokana na kuonesha mapenzi yao juu ya klabu ya Yanga.

Ofisa habari huyo wa Simba alisema moja ya njia ambazo wanatumia wajumbe hao katika kamati hiyo, ni kupiga kura na kitendo cha wajumbe wa kamati hiyo kuwa na mapenzi na Yanga kina lenga kutowatendea haki mabingwa hao wa ligi kuu.

Kamati hiyo ya Mgongolwa inaundwa na wajumbe saba, ambapo mapendekezo hutolewa kwa idadi ya wajumbe kufikia nusu yao kujumlisha mmoja.

Super Star lilimtafuta Katibu Mkuu wa TFF, Angetile Osiah, ili kuthibitisha juu ya taarifa hizo za pingamizi, alisema ofisi yake imepokea pingamizi moja ya Simba juu ya Yondani na Twite, kwa upande wa wajumbe Kamati ya Utendaji alidai hajapokea.

“Nimepokea pingamizi la Simba juu ya Yondani na Twite, na si vinginevyo,” alisema Osiah. 

Kwa upande mwingine, Osiah alishindwa kulitolea ufafanuzi pingamizi la Simba kwa Twite kutokana na timu hiyo kutowasilisha jina lake katika fomu za usajili, hivyo kudai suala hilo litasikilizwa na Kamati ya Katiba.

No comments