Header Ads

ad

Breaking News

Atletico yachafua hali ya hewa Jangwani

 Mchezaji wa timu ya Yanga Juma Abdul akijaribu kunyang'anya mpira kutoka kwa beki wa timu ya Atletico Henry Mbazumutima kwenye  mchezo wa pili wa fungua dimba katika michuano ya kombe la Kagame inayoandaliwa na shirikisho la vyama vya mpira wa miguu Afrika Mashariki CECAFA inayofanyika jijini Dar es salaam Tanzania, Mpira umekiwasha na timu ya Yanga imeambulia kipigo cha magoli 2-0 yaliyofungwa na mchezji Didier Kavumbagu wa Atletico
 Wachezaji wa timu za Yanga ya Tanzania na Atletico ya Burundi wakichuana vikali katika mchezo wao uliofanyika kwenye uwanja wa Taifa jioni ya leo.
 
 
MABINGWA wa michuano ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, maarufu kama Kombe la Kagame, Yanga, wameanza vibaya kampeni ya kutetea ubingwa wao huo baada ya kufungwa mabao 2-0 na Atletico ya Burundi katika mchezo uliofanyika jana kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Kipigo hicho kimekuja wakati klabu hiyo leo ikifanya uchaguzi wa kuziba nafasi zilizo wazi baada ya baadhi ya viongozi wake, akiwamo Mwenyekiti Lloyd Nchunga kujiuzulu.

Bila shaka, kipigo hicho kitakuwa kimetia doa kampeni za baadhi ya wagombea wa uchaguzi wa leo ambao walikuwa wakijinadi kwa wanachama wao kutokana na usajili walioufanya, waliouita ‘wa mauaji’.

Tofauti na matarajio ya wapenzi wa Yanga, timu yao jana ilicheza katika kiwango cha chini mno, wakionekana kuwa wachovu hivyo kushindwa kuhimili mikimikiki ya Atletico.

Pamoja na kuanza vyema mchezo huo, kadri muda ulivyokwenda, wachezaji wa Yanga walizidi kuchoka na baadhi yao kujikuta wakikaba kwa macho.

Kwa kiasi kikubwa, mabadiliko yaliyofanywa kwa upande wa beki wa kulia, Juma Abdul aliyeumia na nafasi yake kuchukuliwa na Ladislaus Mbogo, yalionekana kuigharimu zaidi Yanga kwani wapinzani wao walitumia nafasi hiyo kuelekeza mashambulizi kupitia upande huo wa kulia na kupata mabao yote mawili.

Kwa ujumla, Yanga jana ilizidiwa mno na Atletico ambao walijaza viungo mahiri na wenye nguvu kama Claude Nahimana, Christian Mbilizi aliyeingia kipindi cha pili, Henry Mbazumutima, Gael Duhayingavyi na wengineo.

Pia, washambuliaji wa Atletico kama Didier Kavumbagu aliyefunga mabao yote mawili na Christopher Ndayishimye, walikuwa ni moto wa kuotea mbali kwa mabeki wa Yanga, wakiwa na nguvu, stamina na vimo virefu vilivyowawezesha kumiliki kirahisi mipira ya juu dhidi ya walinzi wa Yanga.

Kwa upande wa Yanga, viungo wake walionekana kuchoka, hasa wale wakabaji ambao muda mwingi walikuwa wakiumaliza katika eneo lao badala ya kupandisha timu hata pale walipokuwa nyuma kwa bao 1-0.

Rashid Gumbo hakucheza kama ilivyo kawaida yake, kama ilivyokuwa kwa Haruna Niyonzima ambaye mara nyingi alikuwa akikaa muda mrefu na mpira kutokana na viungo wenzake kuchelewa kufungua nafasi, lakini wakati mwingine akifanya hivyo kutokana na kujiamini kupita kiasi na mwisho wa siku kujikuta akipokwa mpira au kuupoteza.

Shamte Ally aliyekuwa akicheza kama kiungo wa kulia, hakutoa mchango wowote kama kiungo kwani muda mwingi alikuwa akicheza pembeni ambapo alishindwa kufanya lolote kwani hakuna krosi yoyote ya maana aliyopiga, hilo likitokana na uzito na kutokuwa makini, pale alipopata mpira.

Jerry Tegete aliyekuwa mshambuliaji wa kati wa Yanga, hakufanya kile kilichotarajiwa na wapenzi wa Yanga kutokana na kukosa ushirikiano kutoka kwa viungo wake, ambao mara nyingi walikuwa wakimpelekea mipira miguuni badala ya kwenye njia.

Hamis Kiiza aliyekuwa mshambuliaji mwenza wa Tegete, naye jana hakuweza kufurukuta mbele ya mabeki wa Atletico ambapo hakuwa akitoa msaada wowote kwa timu pale aliopoteza mpira bahati mbaya hata kizembe.


Kwa ujumla, Yanga jana haikucheza kiushindani wakiwa kama mabingwa watetezi hali inayozua hofu iwapo timu hiyo inaweza kutetea ubingwa wake.

Yanga: Yaw Berko, Juma Abdul/Ladislaus Mbogo, David Luhende, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Kelvin Yondani, Athuman Idd ‘Chuji’, Shamte Ally, Rashid Gumbo/Nizar Khalfan, Jerry Tegete/Said Bahanuzi, Hamis Kiiza na Haruna Niyonzima.


Atletico: Said Ndikumana, Francis Nongwe, Hassan Habizimana, Emery Nimubona, Pierre Kwizera, Gael Duhayindavyi, Claude Nahimana/Christian Mbilizi, Henry Mbazumutima/Ciza Hussein, Christopher Ndayishimye, Didier Kavumbagu na Etienne Karekezi.
 

No comments