Header Ads

ad

Breaking News

Yanga yazima kelele za Azam

Haruna Niyonzima
Na Mwandishi Wetu 
YANGA, jana ilizidi kuziwashia taa ya kijani Simba na Azam FC, baada ya kutoka Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam kwa ushindi wa bao 1-0, bao lililofungwa na kiungo wa kimataifa, Haruna Niyonzima katika Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
Hiyo ni ishara nzuri kwa wana Jangwani ambao msimu huu wamepania kuwapoka ubingwa mahasimu wao wakubwa Simba, hasa baada ya kufanya maandalizi ya kutosha ya kuweka kambi nchini Uturuki.
Matunda ya kambi hiyo yameanza kuonekana, hasa baada ya mechi yake ya jana kuonesha soka zuri la kuvutia mbele ya mashabiki wake waliofurika uwanjani hapo. 
Yanga walianza kwa kulisakama lango la Azam FC, ambapo dakika ya sita, Hamis Kiiza, alipata nafasi nzuri na kupiga shuti kali lililodakwa na kipa Mwadin Ali.
Shambulizi hilo liliwazindua Azam FC, dakika ya 10, Kipre Tchetche alijaribu kwa shuti kali, lakini lilitoka nje, wakati tayari kipa wa Yanga, Ally Mustapha ‘Barthez’ akiwa tayari amepotea langoni kwake. 
Dakika ya 16, Kiiza alimpasia pasi nzuri Jerryson Tegete akiwa amebaki na kipa, lakini shuti lake kali lilitua mikononi mwa kipa Mwadin Ally.  
Wakicheza soka zuri la kuvutia, Yanga walipata nafasi nzuri na kulifikia lango la wapinzani wao, lakini beki Joackim Atudo alifanya kazi nzuri ya kuokoa mpira uliopigwa na Simon Msuva na kuwa kona tasa.
Dakika ya 32, Haruna Niyonzima, aliwainua vitini mashabiki wa Yanga baada ya kuifungia timu yake bao zuri la kiufundi.
Tegete siku ya jana haikuwa yake, kwani dakika ya 42 na 43, alishindwa kuipatia timu yake mabao, badala yake akawa anaokoa, baada ya kushindwa kuunganisha mpira wavuni uliopigwa na Haruna Niyonzima.
Yanga ambao walitawala mchezo kipindi chote cha kwanza, kama wangekuwa makini wangeweza kujipatia mabao zaidi ya matatu, lakini washambuliaji wake hawakuwa makini kukwamisha mpira wavuni.
Kipindi cha pili, Azam iliingia kwa lengo moja la kusaka bao la kusawazisha, dakika ya 65, Barthez alifanya kazi ya ziada ya kupangua shuti kali lililopigwa na Kipre Tchetche. 
Wakiwa na uchu za kusawazisha, Kipre Tchetche alipata nafasi nyingine dakika ya 72, lakini shuti lake lilipanguliwa na kipa Barthez, mpira ambao ulitua miguuni kwa Oscar Joshua na kuutoa na kuwa kona tasa.
Pamoja na kipindi cha pili kubadilika na kuliandama lango la Yanga, lakini washambuliaji wa Azam FC walikumbana na ukuta mgumu uliokuwa chini ya Kelvin Yondan na Nadir Haroub ‘Cannavaro’, ambao walikuwa na kazi moja tu, ya kuondosha hatari langoni kwao.
Kwa ushindi huo, Yanga imezidi kuziwashia taa za kijani, Azam na Simba, ambazo ziko katika nafasi ya kufukuzia ubingwa, ikiziacha kwa pointi tatu na nyingine pointi nane.
Baada ya mchezo huo kumalizika, Mwamuzi Hashim Abdallah wa Dar es Salaam alisindikizwa na askali waliokuwa wakilinda usalama uwanjani hapo, wakihofia kufanyiwa fujo na mashabiki.
Yanga: Ally Mustapha ‘Barthez’, Mbuyu Twite, Oscar Joshua, Nadir Haroub Cannavaro, Kelvin Yondan, Athuma Idd ‘Chuji’Simon Msuva, Frank Domayo, Jerryson Tegete/Didier Kavumbagu, Hamis Kiiza/Said Bahanunzi, Haruna Niyonzima.
Azam FC: Ali Mwadin, Kipre Balou/Jabir Aziz, Waziri Salum, Joackin Atudo, David Mwantika, Ibrahim Mwaipopo, Abubakari Salum ‘Sure Boy’, John Bocco, Kipre Tchetche, Hamphrey Mieno, Mcha Hamis.

No comments