Header Ads

ad

Breaking News

Nani kubeba ubingwa wa Bara msimu huu?



LIGI Kuu Tanzania Bara msimu wa mwaka 2011/2012 unanza kutimua vumbo leo, ambapo jumla ya vilabu 14 vitaumana katika mechi za fungua dimba.

SIMBA
Mabingwa watetezi wa ligi hiyo Simba, watakuwa Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, kufungua dimba dhidi ya African Lyon pia ya jiji hilo.
Simba ambao Jumanne ya wiki hii waliichapa Azam FC mabao 3-2 na kunyakua Ngao ya Jamii, wanapewa nafasi kubwa ya kufanya vizuri kwenye msimu mpya wa ligi hiyo, ingawa wanaonekana kuwa na udhaifu katika safu ya ulinzi na kiungo mkabaji.
Pamoja na hilo, lakini timu hiyo inaonekana kuwa na makali ya kutisha kwenye idara ya ushambuliaji.
Kwenye safu hiyo ya ushambuliaji, kuanzia viungo wa kati na pembeni, kuna wachezaji wakali kama Mrisho Ngassa, Emmanuel Okwi, Danniel Akuffo, Abdallah Juma, Felix Sunzu na Haruna Moshi ‘Boban’.
Kikosi hicho ambacho kinanolewa na kocha kutoka Serbia Milovan Cirkovic, kimechukua taji hilo la Tanzania Bara mara 18.

Yanga
Mahasimu wakubwa wa Simba, Yanga, ambao wanashikilia rekodi ya kuchukua ubingwa wa ligi hiyo mara 22, nao wanapewa nafasi kubwa ya kutwaa ubingwa kuliko hata mahasimu wao hao.
Hiyo ni kutokana na usajili mzuri waliofanya msimu huu, tena kwa kuchukua vijana wengi wazuri kutoka hapa nchini.
Na hata usajili wao kwa upande wa wachezaji wa kigeni, imekuwa ni tofauti na miaka iliyopita, kwani miaka ya nyuma walikuwa wakinunua wachezaji kwa gharama kubwa tofauti na viwango vyao.
Mmoja wa wachezaji wa kigeni ambao walinunuliwa na Yanga misimu iliyopita, huku wakiwa na viwango vibovu ni Jama Mba Robert kutoka Cameroon.
Kwa sasa Yanga imesajiliwa ‘mawe’ ya ukweli kutoka ugenini, ambao ni Mbuyu Twite wa FC Lupopo ya DR Congo, Didier Kavumbangu kutoka Atletico ya Burundi, huku ikiwa na wageni wengine hatari kama Haruna Niyonzima (Rwanda) na Hamisi Kiiza (Uganda).
Kwa upande wa wachezaji wa nyumbani, wamewasajili akina Said Bahanunzi kutoka Mtibwa Sugar, Ally Mustafa ‘Barthez’ (Simba), Juma Abdul, David Luhende (Kagera) Sugar, Kelvin Yondan (Simba), Frank Domayo (Ruvu Shooting), Simon Msuva na Nizar Khalfan.
Kwa wachezaji hao ukichanganya na wale wa zamani kama akina Athumani Iddi ‘Chuji’, Juma Seif ‘Kijiko’, Shamte Ally, Jerryson Tegete, Job Ibrahim, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Rashid Gumbo na Nurdin Bakari, ni wazi Yanga wataleta ushindani mkubwa kama si kuipora Simba ubingwa, baada ya msimu uliopita kushika nafasi ya tatu.

AZAM FC
Azam hawajafanya usajili wa kutisha kwenye kikosi chao msimu huu zaidi ya kumwongeza mlinda mlango Deogratias Munishi ‘Dida” kutokana Mtibwa Sugar ili kusaidiana na kipa mwingine Mwadini Ally.
Kikosi hicho cha Azam, kama kitakuwa makini, nacho kinaweza kunyakua ubingwa wa ligi hiyo, kwa kuwa ni kikosi kizuri ambacho kimeonesha upinzani mkubwa msimu uliopita na kushika nafasi ya pili.
Klabu hiyo yenye makazi yake Chamazi, nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam, pamoja na kuwa na miaka sita tu kwenye ligi hiyo, imeonekana kuwa kivutio na washindani wa kweli kwenye ligi hiyo.
Kwa kutokufanya usajili, hakuwafanyi kukosa nafasi ya kutwaa ubingwa, kwa kuwa bado wana kikosi kizuri kinachotandaza soka safi.
Azam wanawategemea zaidi washambuliaji wao John Bocco na Kipre Tchetche raia wa Ivory Coast, ambao wamekuwa mwiba mchungu kwa timu pinzani katika mechi kadha wa kadha.
Katika kiungo, kuna vipaji kama Abdi Kassim ‘Babi’, Ibrahim Mwaipopo, Abdulrahim Humoud, Salum Abubakari (Sure Boy Jr), Himid Mau na wengineo.
Pamoja na wachezaji hao, Azam ina ukuta mzuri unaoundwa na kuongozwa na nahodha Aggrey Morris, Said Morad na Erasto Nyoni ambaye kwa sasa kiwango chake ni cha juu mno.

Mtibwa SUGAR
Tangu mwaka 2000 Mtibwa wachukue taji la ligi hiyo, haijaonyesha makali yake, lakini wamekuwa wakitoa upinzani mkubwa kila msimu.
Nafasi ya kikosi hicho cha Mtibwa kutwaa ubingwa si kubwa sana, ingawa wanatarajiwa kutoa upinzani kama misimu mingine iliyopita.
Mtibwa wamemuongeza mchezaji aliyewahi kuichezea klabu hiyo zamani, Shaaban Kisiga na kumrejesha Shaaban Kado aliyekuwa Yanga, ambao wataungana na wachezaji wengine kama Shaaban Nditi na Hussein Javu kuhakikisha wanafanya vizuri msimu huu.

COASTAL UNION
Ukiachana na Mtibwa, timu ya Coastal Union ‘Wagosi Wakaya’ ya Tanga, nayo inatarajiwa kuleta upinzani mkubwa kutokana na jinsi walivyojipanga, baada ya kuonyesha cheche zao mzunguko wa pili msimu uliopita.
Klabu hiyo ilivurunda vibaya katika msimu wa kwanza wa ligi hiyo na kupokea vipigo vya mbwa mwizi kama kile cha mabao 5-0 dhidi ya Yanga.
Lakini mzunguko wa pili, mabingwa hao wa mwaka 1988, walibadilika na kutoa vipigo na kuwafanya kushika ya tano kwenye ligi hiyo.
Klabu hiyo yenye maskani yake Barabara ya 11 mjini Tanga, inapewa nafasi kubwa ya kuleta upinzani kwenye kinyang'anyiro cha kuwania taji hilo la Tanzania Bara.
Kikosi chao kimefanya usajili 'bab kubwa' kwa kuwasainisha nyota kama Mkenya Jerry Santo, Razak Khalifan, Kassim Seleman ‘Selembe’, Nsa Job, Green Atupile na Juma Jabu aliyetokea Simba.

Kagera Sugar
Kagera Sugar nayo ni moja ya timu zinazotoa upinzani mkuwa kwenye ligi hiyo, huku ikiwa na kikosi kilichomudu kubaki kwenye kiwango kizuri ingawa hakijawahi kuchukua ubingwa.
Timu hiyo yenye yenye makazi yake kwenye mashamba ya miwa ya Kagera, msimu huu imewasajili wachezaji kama Enyinna Darlinton na Benjamin Ese Fuyo wote kutoka Nigeria, Salum Kanone (Moro United), Malika Ndeule na Zuberi Dabi (Villa Squad).

JKT RUVU, JKT OLJORO
NA  RUVU SHOOTING
JKT Ruvu, Ruvu Shooting na JKT Oljoro ni timu ambazo zilionesha soka safi, japokuwa hazikuweza kufanikiwa kufanya mambo makubwa katika msimu uliopita.
JKT Ruvu wamemsajili Credo Mwaipopo na Mussa Hassan ‘Mgosi’, jambo linalowapa matumaini ya kuweza kufanya vizuri kwenye ligi hiyo, ingawa si kuchukua ubingwa.
Kwa upande wa Ruvu Shooting watakuwa na wakati mgumu kuweza kukaa sawa kwenye msimu huu wa ligi, baada ya kuwauza wachezaji wake muhimu.
Ruvu imemuuza Abdallah Juma na Paul Ngalema kwenda Simba, huku kiungo Frank Damayo akitua Yanga.
Oljoro wameweza kubaki kwenye kwenye ligi hiyo, baada ya kupanda msimu uliopita, huku wakionesha soka safi ingawa nao hawana nafasi ya kutwaaa upingwa.

African Lyon
African Lyon si timu ya kuchukua ubingwa nah ii inatokana na madai ya uongozi wa klabu hiyo, kuwa wao wako kwenye ligi kuu ya bara kwa ajili ya kuinua vipaji.

Toto African
Hali hiyo ipo pia kwa Toto African, ambao nao wamekuwa wakijiandaa msimu mzima kwenye ligi kwa ajili ya kuifunga Simba na si kuleta ushindani wowote kwenye ligi.

Polisi Moro, Prisons NA JKT Mgambo
Timu zilizobaki ni zile zilizopanda daraja msimu huu, ambazo ni Polisi Moro, Prisons ya Mbeya na JKT Mgambo ya Tanga.
Kwa klabu hizo kwa sasa zitakuwa zikifikiria kubaki kwenye ligi hiyo kwanza na si kufikiria kuchukua nafasi ya juu.
Kwa upande wake, Prisons huenda ikawa tofauti kwa kuwa ni timu yenye uzoefu mkubwa na ligi hiyo, hivyo inaweza ikatoa upinzani kwa vigogo wa ligi hiyo.

No comments