Header Ads

ad

Breaking News

Yanga mwendo mdundo, yaichapa Express 2-1, Tegete shujaa



KAMA si juhudi zako Manji, Kama si juhudi zako Manji, leo hii Yanga ingekuwa wapiiiii. Hicho ni kibwagizo cha wimbo kilichokuwa kikiimbwa na watani wao wa jadi, mashabiki wa Simba, wakati wa mechi ya kirafiki ya kimataifa kati ya Yanga na Express ya Uganda.

Mabingwa wa kombe la klabu bingwa Afrika Mashariki na Kati (Kombe la Kagame), Yanga jana waliibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Express, katika mchezo wa kirafiki wa kimataifa uliopigwa Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Wakiwa na furaha, huku wakishuhudia silaha zao mpya zilizosajiliwa kwa ajili ya Ligi Kuu Bara msimu ujao, Yanga walianza mchezo kwa kasi na kufanikiwa kupata bao la kwanza dakika ya tatu likifungwa na Jerryson Tegete, baada ya kazi nzuri iliyofanywa na Salum Telela.
Yanga wafanikiwa kupata bao la pili  dakika ya 19, lililofungwa na Tegete kwa kichwa  baada ya kazi nzuri iliyofanywa na Said Bahanuzi.

Bahanuzi aliyetokea Mtibwa Sugar, aliwapangua mabeki wa Express na kupiga mpira uliosindikizwa wavuni na Tegete ambaye msimu uliopita alikuwa hachezeshwa mara kwa mara na kocha aliyeondoka Mserbia Kostadin Papic.

Katika mchezo huo, Express ilishindwa kuonesha makali yake kipindi cha kwanza, lakini walionekana kuwasoma zaidi wapinzani wao, ambapo dakika ya 39, walibadilika na kuanza kuonana vizuri huku wakimjaribu kipa wa Yanga, Ally Mustapha ‘Barthez’ aliyetokea timu ya Simba.

Express wakiingia kipindi cha pili wakiwa wamebadilika, walifanikiwa kulifikia lango la Yanga na dakika ya 52, Joseph Kayira alikosa bao baada ya mpira wa adhabu aliopiga ulipanguliwa na kipa Barthez na kuwa kona ambayo haikuzaa matunda.

Dakika ya 73, Kayira aliisawazishia bao timu yake ya Express kwa kichwa akitumia vizuri mpira wa adhabu uliopigwa na Suleiman Jingo aliyeingia kuchukua nafasi ya Mike Masaba.
Express pamoja na kuonesha kiwango kizuri cha soka, walikosa mabao matatu kipindi cha pili, huku mashabiki wa soka wanaokaa upande unaopendelewa na Simba, wakiinua kushangilia wakidhani ni bao.

Mpira huo ulichelewa kuanza baada ya Express kutaka fedha zao, lakini Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), lilielewana nao na kukubali kuingia baada ya kupewa sh. milioni sita na waandaaji wa mchezo huo.

Express walikuwa wakilalamika kwani mwaka juzi kampuni moja iliwaalika mkoani Mwanza, lakini mpaka wanamaliza ziara yao, hawakulipwa fedha walizokubaliana nao, ndiyo maana wakaamua wapewa kabla ya kuanza kucheza mechi hiyo.

Yanga inajiandaa na mechi za Kombe la Kagame zitakazoanza Julai 14, mwaka huu jijini Dar es Salaam na Ligi Kuu Bara.

Mchezo huo ulisimama dakika tatu, baada ya Stephano Mwasyika kuingia huku akiwa amefungiwa na TFF, baada ya kumpiga mwamuzi Israel Mujuni, lakini waamuzi waliokuwa wakichezesha mechi hiyo, baada ya kujadiliana, walimruhusu na kuendelea na mchezo.

Yanga: Ally Mustapha ‘Barthez’, Juma Abdu, Oscar Joshua/Stephano Mwasyika, Kelvin Yondani, Nadir Horoub ‘Cannavaro, Athuman Idd ‘Chuji’, Nizar Khalfan/Shamte Ally, Salum Telela, Frank Domayo, Said Bahanuzi, Simon Msuva/Idrisa Rashid.

No comments