Header Ads

ad

Breaking News

Simba teja la Mtibwa Sugar, yapigwa 1-0 U/Taifa

Juma Kaseja, kipa wa Simba
KWELI sikio la kufa halisikii dawa; hivyo ndivyo tunavyoweza kusema, baada ya mabingwa wa soka nchini Simba, kukubali kipigo cha bao 1-0 dhidi ya Mtibwa Sugar ya mkoani Morogoro.
Kipigo hicho ni kama mwendelezo wa uteja, kwani katika mechi ya kwanza iliyopigwa kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro, Simba ilichapwa mabao 2-0, hivyo Mtibwa kwa msimu huu wametwaa pointi zote sita kutoka kwa Simba.
Mchezo huo ulianza kwa timu zote kusoma, huku zikicheza zaidi sehemu ya katikati ya uwanjani kwa kuwaacha viungo kuonesha uwezo wao wa kumiliki na kugawa mipira kwa wenzao.
Mtibwa Sugar, ndio waliokuwa wa kwanza kulifikia lango la Simba na kujipatia bao dakika ya 19, lililofungwa na beki Salvatory Ntebe aliyetumia vizuri pasi ya Shaaban Kisiga.
Bao hilo lilianzia kwa mpira wa kona uliopigwa na Rashid Gumbo na kuokolewa na Koman Billi Keita, lakini ukatua kwa Kisga aliyemskumia pasi nzuri mfungaji wa bao hilo.
Dakika tano baadaye, Hussein Javu alishindwa kuifungia timu yake bao, baada ya kuwatoka mabeki wa Simba na kupiga shuti kali lililodakwa na kipa Juma Kaseja.
Simba walijibu mashambulizi hayo na kulifikia lango la wapinzani wao, lakini Mzambia Felix Sunzu, alishindwa kuisawazishia bao timu yake baada ya mpira wa kichwa aliopiga kuokolewa.
Wakati mabadiliko yakifanyika kwa upande wa Simba, Mrisho Ngassa akiingia kuchukua nafasi ya Haruna Chanongo, mashabiki wa Yanga, waliamka kwa furaha na kumshangilia huku wakiimba, Ngassa, Ngassa, Ngassa.
Hiyo ni mara ya pili, kwani mwaka jana wakati Azam ilipocheza mechi za Kombe la CECAFA, wakati mpira ulipomalizika, mashabiki wa Yanga walimshangilia na kumvalisha jezi ya Yanga na kusababisha mtafaruku na timu yake.
Simba walipata pigo dakika 85, baada ya beki wake wa kati, Juma Nyosso kutolewa nje kwa kuoneshwa kadi nyekundu na mwamuzi Ibrahim Kidiwa kutoka Tanga, baada ya kumchezea vibaya Vicent Barnabas wa Mtibwa Sugar.
Kwa matokeo hayo, Simba imebaki katika nafasi tatu ikiwa na pointi zake 33, wakati Mtibwa Suga ikipanda hadi nafasi ya sita, baada ya kujikusanyia pointi 27.
Simba: Juma Kaseja, Nassoro Cholo, Amir Maftah, Juma Nyosso, Koman Billi Keita, Shomari Kapombe, Ramdhan Chombo ‘Redondo’/Kigi Makassy, Mwinyi Kazimoto, Felix Sunzu, Haruna Moshi ‘Boban’/Amri Kiemba, Haruna Chanonga/Mrisho Ngassa.
Mtibwa: Hussein Sharifu, Said Mkopi, Issa Rashid, Salvatory Ntebe, Salum Swedi, Shaaban Nditi, Jamal Mnyate, Rashid Gumbo, Hussein Javu/Juma, Shaaban Kisiga, Vicent Barnabas.

No comments