Header Ads

ad

Breaking News

Hukumu ya Yondani, Twite leo



*Klabu zaitwa TFF kutoa, kutetea hoja


HUKUMU ya wachezaji waliowekewa pingamizi na klabu mbalimbali za Ligi Kuu Tanzania Bara, itatolewa na Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji itakayokutana leo jijini Dar es Salaam, huku Kelvin Yondani na Mbuyu Twite, wakigonganisha vichwa vya wengi.

Akizungumza jijini Dar es Salaam jana, Ofisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Boniface Wambura, alisema kuwa, kamati hiyo ilikutana juzi na kuamua kuziita klabu zote zilizoweka na kuwekewa pingamizi ili zikisilikilizwe.

“Kamati imeziita timu zote zilizoweka na kuwekewa pingamizi ili zisiwasilishe hoja zao na zilizowekewa zijibu hoja,” alisema.

Wachezaji hao wamepingwa na Simba kwa maelezo kuwa waliwasajili, hivyo wanastahili kuitumikia klabu hiyo kongwe nchini, badala ya kuichezea Yanga katika msimu mpya wa ligi kuu.

Wambura alisema mpaka sasa hakuna pingamizi lolote lililotolewa uamuzi, kwani kamati ndiyo yenye maamuzi ya mwisho, ambapo inakutana leo chini ya Mwenyekiti wake Alex Mgongolwa.

Pingamizi linalosubiriwa na mashabiki wa soka ni la Kelvin Yondan aliyeihama Simba na kutua Yanga na  Mbuyu Twite aliyetoka FC Lupopo ya DR Congo, lakini msimu uliopita akiichezea APR ya Rwanda kwa mkopo.

Mchezaji mwingine aliyekewa pingamini na timu yake ya zamani ni Ramadhan Chombo ‘Redondo’,  aliyesaini kuichezea Simba, akitokea Azam FC pamoja na wachezaji wote wa kigeni wa Simba, waliowekewa pingamizi na mahasimu wao, Yanga.

Wachezaji wa kigeni waliowekewa pingamizi kwa madai kuwa, walikuwa na leseni ya kucheza soka iliyotolewa na  Shirikisho la soka Tanzania (TFF), ambao wanaichezea Simba ni Felix Sunzu, Emmanuel Okwi, Mussa Mudde, Koman Billi Keita, Pascal Ochieng, Daniel Akuffo, Lino Musombo na Kanu Mbiyavanga na Mtanzania Danny Mrwanda.

Kwa upande wa Yanga, wachezaji waliopinga Mbuyu Twite na Kelvin Yondan, ambao wanadaiwa walisaini kuichezea timu hiyo. Hata hivyo, Yondan katika michuano ya Afrika Mashariki na Kati (Kombe la Kagame), aliruhusiwa  kuichezea Yanga.

Wakati huo huo, Wambura alisema kuwa, uongozi wa klabu ya Simba, uliwasilisha barua ya makubadiliano na Azam FC ya kuwaachia Redondo, kwa ada ya uhamisho wa sh. milioni 25.

Wambura alisema kuwa, baada ya barua hiyo, TFF ilipokea barua pepe kutoka katika klabu ya Azam ikielezea suala hilo, lakini walishindwa kuifanyia kazi, kutokana na kukosa viambatanisho muhimu vya klabu hiyo ambavyo vinaonyesha kweni inatoka Azam.

“Azam walituandikia barua pepe kutujulisha makubaliano yao na Simba, lakini haikukamilika, hivyo haikufanyiwa kazi mpaka watakaporekebisha, lakini iwe kabla ya kamati kuketi,” alisema.

SuperStar lilimtafuta Ofisa Habari wa Azam FC, Jaffar Idd, ambaye alisema kuwa, wamekubaliana na Simba na tayari wamekabidhiwa sh. milioni 10 za utangulizi, na kuahidiwa kumaliziwa sh. milioni 15, wakati wa mechi ya Ngao ya Jamii,  Septemba 11 mwaka huu.

“Simba tumemalizana kuhusu Redondo, wametutangulia sh. milioni 10, nyingine wametuahidi wakati wa mechi ya Ngao ya Jamii,” alisema.

Lakini, alipoulizwa kuhusu barua pepe waliyotuma TFF, alisema kuwa, hana maelezo zaidi ya hayo ya kukubaliana.

No comments