Header Ads

ad

Breaking News

Yanga yatuma salamu timu zitakazoshiriki Kagame

Yanga
MABINGWA wa soka Afrika Mashariki na Kati, Yanga, wametuma salamu kwa timu zitakazoshiriki michuano ya Kombe la Kagame baada ya jana kuichezesha samba la Kispania, JKT Ruvu katika mchezo wa kirafiki uliofanyika kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Katika mchezo huo, Yanga ilishinda mabao 2-0 yaliyofungwa na beki Nadir Haroub ‘Cannavaro’ na mshambuliaji Hamis Kiiza akitokea benchi.

Mbali ya ushindi huo, kiwango kilichoonyeshwa na Yanga jana ndicho hasa kilichowachengua mashabiki wake ambao muda wote wa mchezo huo dhidi JKT Ruvu wanaosifika kwa soka la kitabuni, walikuwa wakishangilia soka iliyoonyeshwa na vijana wao hao.

Na kwa kuwa wakongwe hao wa soka nchini walikuwa wakicheza na timu inayojua kusakata kandanda hasa, haikuwa shida kwa vijana wa Jangwani kuonyesha uwezo wao uwanjani hapo.

Japo timu hiyo imeanza kambi hivi karibuni tofauti na JKT Ruvu ambao huwa wapo kambini kwa muda mrefu, vijana wa Jangwani hawakupata shida dhidi ya wapinzani wao kuonyesha nini wamevuna ndani ya muda huo mfupi, chini ya Kocha Mkuu Mbelgiji Tom Saintfiet na msaidizi wake, Fred Felix Minziro.

Miongoni mwa wachezaji waliong’ara jana ni kiungo Mnyarwanda Haruna Niyonzima, Kiiza, Rashid Gumbo, Nizar Khalfan, beki mpya wa pembeni David Luhende, Kelvin Yondani aliyejiunga na timu hiyo akitokea Simba, Juma Abdul, Jerry Tegete na wengineo. 

Kati ya wote hao, Niyonzima ndiye aliyechengua zaidi uwanjani hapo kutokana na ufundi wake katika kuchezea mpira, pasi ‘zilizokwenda shule’, na zaidi ikiwa ni uwezo wake wa kutumia akili awapo na mpira.

Kwa kiasi kikubwa, Niyonzima ndiye aliyekuwa nyota wa mchezo wa jana, huku akifuatiwa na Luhende ambaye alionyesha kiwango cha hali ya juu katika nafasi aliyocheza ya beki wa kushoto, zaidi ikiwa ni katika kupiga krosi kwa ufundi wa hali ya juu.

Niyonzima alikuwa akiwasunguka kama alivyotaka wachezaji wa JKT Ruvu, ikiwa ni pamoja na kupiga krosi iliyozaa bao la pili lililofungwa na Kiiza kwa kifua na hivyo kuwapagawisha wapenzi wa timu hiyo.

Kwa upande wake, Gumbo ambaye alikuwa akisotea benchi enzi za Kocha Kostadin Papic, jana aliwaonyesha wapenzi wa timu hiyo kile walichokuwa wakikikosa kutoka kwake kutokana na jinsi alivyokuwa akitamba katika eneo la kiungo akishirikiana na Niyonzima, Nizar, Athuman Idd ‘Chuji, Tegete, Said Bahanuzi na wengineo.

Kwa ujumla, Yanga jana walionyesha dalili nzuri ya kufanya vyema katika michuano ya Kombe la Kagame kutokana na uchezaji wao kupitia mfumo wa 3:5:2 na wakati mwingine 3:5:1:1.






No comments